SIMU ZA WATU MILIONI NANE KUFUNGIWA MWISHO MWA MWEZI HUU

WATUMIAJI wa simu wapatao milioni nane wapo hatarini kufungiwa simu zao ifikapo mwishoni mwa mwezi huu, Tanzania Daima limebaini.

Tayari Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeziandikia kampuni za simu waraka wa kuzitaka zianze kukata kodi mpya ya laini (simu card) mara moja kuanzia Julai 30, 2013.


Hatua hiyo inatokana na serikali kushindwa kufuta kodi hiyo ya sh 1,000 iliyopitishwa na Bunge kama alivyoagiza Rais Jakaya Kikwete baada ya kukutana na wadau wa sekta ya mawasiliano.

Kwa maana hiyo kila anayemiliki laini moja ya simu atakatwa sh 3,000; anayemiliki laini mbili sh 6,000 na anayemiliki laini tatu sh 12,000, lengo ni kuhakikisha serikali inakusanya sh bilioni 178 zitakazopelekwa kwenye bajeti kuu ya serikali.

Watumiaji wa simu sasa watalazimika kulipia kodi hiyo ya miezi mitatu ya Julai, Agosti na Septemba kwa wakati mmoja.

Bunge kupitia Kamati ya Bajeti inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge (CCM) lilitaka kuwapo kwa kodi hiyo ili kusaidia shughuli za bajeti ya Serikali Kuu.

Kupitishwa kwa kodi hiyo kuliibua malalamiko ya wanasiasa dhidi ya Chenge anayelazimisha kuwapo kwa kodi hiyo, huku akishindwa kuamini kwamba kuna Mtanzania anayekosa sh 1,000 kwa mwezi kwa ajili ya laini ya simu.

Malalamiko hayo yaliendelea hadi kwa wananchi na baadhi ya wabunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) waliotaka posho za wabunge zipunguzwe ili kuziba pengo hilo badala ya kuwabebesha wananchi mzigo.

Inadaiwa kwamba msimamo wa Chenge unaungwa mkono na Spika wa Bunge, Anne Makinda, jambo lililosababisha kutojadiliwa kwa hoja binafsi ya Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (CHADEMA) iliyohusu kodi hiyo katika mkutano wa Bunge lililopita kwa kisingizio cha kukosekana kwa muda wa kufanya hivyo.

Hata hivyo, takwimu zilizotolewa na kampuni za simu zinaonyesha kuwa miongoni mwa wamiliki wa laini za simu milioni 22; milioni nane wanatumia chini ya sh 1,000 kwa mwezi.

Baada ya malalamiko hayo, Rais Kikwete alikutana na wadau wa mawasiliano ambao ni wamiliki wa kampuni za simu Tanzania (MOAT), Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Waziri wa Fedha, William Mgimwa, kisha kuwaagiza waiondoe kodi hiyo.

“Rais alisema lengo kuu la mkutano huo liwe kupendekeza jinsi ya kuziba pengo la sh bilioni 178 zitakazopotea katika bajeti iwapo kodi hiyo itafutwa.

“Alisema hawezi kuifuta moja kwa moja kodi hiyo, bila kutafuta njia nyingine za kupata fedha kujazia pengo litakalotokeza huku tayari Bunge limezipangia matumizi,” alinukuliwa Makamba baada ya kikao hicho na rais.

Kwa upande wake, rais alikaririwa akiwaambia wadau hao wa mawasiliano kwamba: “Nakuombeni kaeni pamoja, wekeni bongo zenu pamoja, wekeni akili yenu pamoja tutafute namna gani tutajaza pengo hili la sh bilioni 178 endapo tutakubaliana kuwa kodi hii inawabebesha wananchi mzigo mzito, na kuwa pengine menejimenti ya kodi yenyewe ni ngumu.”

Licha ya agizo hilo la rais kutekelezwa kwa MOAT kutakiwa kuongeza kodi nyingine iitwayo ‘Excise duty’ kutoka asilimia 14 hadi 17 bila kujali kwamba katika Bunge la bajeti kodi hiyo iliongezwa kutoka asilimia 12 hadi asilimia 14, tozo hiyo ya laini za simu haijaondolewa.

Wachambuzi wa masuala ya siasa na mawasiliano walisema kutojadiliwa kwa mabadiliko ya kodi hiyo ya simu ni dalili kwamba Waziri wa Fedha amezidiwa nguvu na kiti cha spika kinachounga mkono hoja hiyo ya Chenge na kushindwa kutekeleza agizo la rais.

Wataalamu wa mawasiliano walilieleza gazeti hili kwamba kuongezeka kwa kodi hiyo kutaifanya Tanzania kuwa na kiwango cha juu cha kodi kuliko nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ushauri wa wataalamu hao ulibainisha kwamba kuongezeka kwa kodi hiyo kunaleta nafuu kidogo kuliko ile ya laini za simu inayomuumiza zaidi mwananchi wa kawaida.

Share this:

Post a Comment

 
Copyright © CHIWILEINC. Designed by OddThemes | Distributed By Gooyaabi Templates