Audio: Stereo awasikitikia wasanii wa hip hop Tanzania, adai aliuza album yake 'African Son' yenye nyimbo 19 kwa shilingi Milioni 1.5 tu

Member wa zamani wa label ya M-Lab ambaye sasa hivi anafanya kazi chini ya Unit Entertainent ameonesha masikitiko yake kwa wasanii wanaofanya hip hop Tanzania kwa kudai kwamba hali ni ngumu na haiwafaidishi wengi hata kwa kiwango cha kawaida.
Mkali huyo aliyeacha alama mitaani kwa baadhi ya wasanii kuiga mitambao yake ‘Stereo flow’, amefunguka wakati akifanya mahojiano na Jabir Saleh aka Kuvichaka ama The Library/Maktaba.

“Ma-rapper wengi hawasemi ukweli, maisha ni magumu sana mtaani.” Amesema Stereo na kujitolea mfano kwamba anaweza kupewa show Mwanza na akaambiwa atalipwa kiasi cha shilingi laki nane, na kwa kuzingatia kwamba yeye ni mwanafunzi anaona ni bora aombe tiketi ya ndege ili aweze kufanya show na kurudi haraka kuendelea na masomo. Lakini promoter akisikia hilo ombi ataahirisha kabisa mpango huo.
Amelinganisha mfano huo na jinsi ambavyo wasanii wa kuimba ama wa bongo fleva wanavyothaminiwa na mapromoter ambao huwaona wasanii wa hip hop kama wasindikizaji kwenye show hizo.
“Lakini ni rahisi sana labda kumpa tiketi ya ndege Shetta aende sehemu flani au sehemu flani. Kwa nini? Labda anaona  kwa Shetta hapotezi. Anaona ‘ah mtu kama Shetta ntampeleka pale, ana watu wengi na anafanya muziki ambao unasikilizwa na watu wengi sana. Hao watu wa hip hop ama michano ni watu wa ziada ziada tu katika show’. Ukiangalia sasa wewe hiyo laki nane ndiyo umepewa inabidi ukachukue hata jeans au hata raba mpya. Ukicheki hadi unaenda kwenye show labda umebaki na laki mbili mfukoni.”
Kwa mahesabu hayo, Stereo anashauri ni bora kuacha muziki! Lakini amedai haiwezekani kwa sababu muziki kwa rappers ni kama ugonjwa.
“Sasa huo muziki unafanya wa kazi gani, unakulipa nini? Ni bora uache, yaani bora kama unasoma soma na kama una kazi zingine fanya. Lakini hatuwezi kuacha muziki. Yaani muziki ni kama ugonjwa yaani, yaani kama mtu ambaye sijui anaumwa kitu gani ambacho hauwezi kupona, mi nafikiri hata Hasheem Dogo hatumsikii kwenye hewa, lakini naamini kuna kitu anafanya, kuna sehemu labda akikaa anaweza kurekodi hata freestyle na nini, huwezi kuacha muziki.” Amefunguka Stereo.
Kilio cha rapper huyo mkali ambaye hivi karibuni ameachia wimbo wenye ujumbe wa mapenzi ‘Usione Hatari’ akiwa na Ben Pol, kilifikia hatua ya kutoa mfano hai wa album yake nzito iliyokuwa imesheheni ngoma kali ‘African Son’ ambayo ni kama ilimvunja moyo kimauzo.
“Watu hawasapoti, nimefanya African Son, 1.5 Million ndicho kitu kilichorudi. Nyimbo 19 sijui 20 zilikuwa.” Alieleza.
“One point five million, One point five million, milioni moja na laki tano.” Alisisitiza kwa masikitiko.
Rapper huyo amewataka wasanii wa hip hip Tanzania kusema ukweli kuhusu hali ngumu iliyoko mtaani. Endelea kufuatilia hapa tutakueleza mbinu alizozieleza Stereo zinazoweza kuwasaidia rappers Tanzania. MSIKILIZE HAPA CHINI

Share this:

Post a Comment

 
Copyright © CHIWILEINC. Designed by OddThemes | Distributed By Gooyaabi Templates