Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Makazi,
Maji na Nishati Nd. Ali Khalil Mirza Kushoto na Mwenzake wa Wizara ya
Kilimo na Maliasili Nd. Afan Othman Maalim wakikabidhiana ahati za
usimamizi wa Mashamba ya Serikali ambayo yalikuwa chini ya usimamizi wa
Wizara ya Ardhi.
Nyuma yao ni Mkuu wa Wilaya ya Chake chake Bibi Mwanajuma Majid.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Ali Iddi akimkabidhi nyaraka za Mashamba ya Serikali Katibu
Mkuu Wizara ya Kilimo na Maliasili Zanzibar Ndu. Afan Othman Maalim
hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Tasaf Ofisi ya Makamu Pili wa Rais
wa Zanzibar Chake Chake Pemba.
Walioshuhudia kati
kati yao ni Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Mh. Dadi Faki Dadi na Mkuu
wa wilaya ya Chake chake Bibi Mwanajuma Majid.
Picha na Hassan Issa OMPR
Na Othman Khamis Ame
Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar imefikia uamuzi wa Mashamba yote ya Serikali yaliyokuwa
chini ya usimamizi na uangalizi wa Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na
Nishati kuanzia sasa yatasimamiwa na Wizara ya Kilimo na Mali asili
Zanzibar.
Hatua hiyo imekuja
baada ya Serikali kuzingatia kwa kina kwamba Wizara ya Kilimo na
Maliasili ndio yenye dhamana ya kusimamia uhuishaji wa miti hasa
mikarafuu na minazi ambayo ndio inayoonekana kusheheni zaidi katika
mashamba hayo.
Hati za makabidhiano
ya usimamizi wa mashamba hayo ya Serikali zilifanyika katika ukumbi wa
Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania { Tasaf } wa Ofisi ya Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar uliopo Chake chake Kisiwani Pemba na
kushirikisha pia watendaji wa Wizara zote mbili.
Katibu Mkuu Wizara ya
Ardhi, Makazi, Maji na Nishati Nd. Ali Khalil Mirza alimkabidhi hati
hizo Katibu Mkuu mwenzake wa Wizara ya Kilimo na Maliasili Nd. Afan
Othman Maalim tukio ambalo lilishuhudiwa pia na Makamu wa Pili wa Rais
wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
Akikabidhi hati hizo
Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati Nd. Ali Khalil
Mirza alisema Wizara hiyo ilikuwa ikidhibiti mashamba 111 ya Eka Tatu
Tatu Unguja na Pemba kuanzia mwaka 1989 ambayo wananchi waliokuwa
wakiyatumia kwa shughuli zao za Kilimo kwa sasa wamefariki Dunia.
Nd. Mirza alisema hati
hizo zilizomo kwenye madaftari Manne zinaonyesha rikodi zote za uwepo
wa mashamba 8,215 ya eka tatu tatu Zanzibar ambazo kwa mujibu wa sera za
mabadiliko ya ardhi zilikuwa chini ya iliyokuwa Kamisheni ya Ardhi na
Mazin gira tokea mwaka 1989.
Akipokea Madaftari
hayo yenye hati za kumbu kumbu za mashamba hayo ya Serikali Katibu Mkuu
Wizara ya Kilimo na Mali asili Nd. Afan Othman Maalim aliwaomba
watendaji wa Wizara ya Ardhi kuendelea kutoa ushirikiano wa utambuzi wa
Mashamba hayo kwa lengo la kulinda Mali za Serikali.
Nd. Afan alifahamisha
kwamba kutokana na umuhimu uliojitokeza hivi sasa wa matumizi makubwa
ya mashamba unaotokana na mabadiliko ya Dunia bila shaka zinaweza
kujitokeza hitilafu na changamoto zitakazohitaji kutatuliwa kwa pamoja
kati ya taasisi hizo.
Mapema Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar kupitia Baraza lake la Mapinduzi iliamua kuunda kamati
Maalum kujaribu kufuatilia kasoro zilizomo za matumizi mabaya ndani ya
mashamba yote ya Serikali.
Balozi Seif
alifahamisha kwamba ripoti ya Kamati hiyo ilithibitisha kwamba mengi ya
mashamba ya Serikali hasa yale yaliyokuwa yalisimamiwa na Wizara ya
Ardhi, Makazi, maji na Nishati yalikosa usimamizi mzuri.
Makamu wa Pili wa Rais
wa Zanzibar alitolea mfano Mashamba mengi ya mikarafuu hasa Kisiwani
Pemba kwa kipindi kirefu yalikosa huduma inayostahili na kusababisha
upungufu wa uzalishaji wa zao la Karafuu.
Post a Comment